HIZI NI SABABU ZA MZUNGUKO WA HEDHI KWA WASICHANA KUBADILIKA!

Tumekuwa tukisikia mambo mengi sana yanayohusu mzunguko wa hedhi kwa wanawake na wakati mwingine hutufanya tudhani kuwa mzunguko huo huenda sana na saa nzima kwamba hauna vikwazo vyovyote.

Wengi wamekuwa wakisema kuwa wanawake wanaopata hedhi kila baada ya majuma manne ndio mzunguko sahihi lakini pengine unaweza kusema kuna vitu kuhusu wanawake ambavyo hatuvifahamu. Kiuhalisia, sio wanawake wote wanapata hedhi katika mzunguko ulio sawa kama ilivyokuwa mara ya mwisho.

Wasichana wengi huanza kupata hedhi kati ya umri wa miaka 10 hadi 15, lakini wachache huanza mapema au huchelewa. Hedhi ya kwanza kwa kitaalamu huitwa menarch.

Wataalamu wengi wa afya huzungumzia mzunguko wa hedhi kwa siku 28, lakini hicho ni kiwango cha wastani ambacho madaktari hukitumia. Urefu wa mzunguko wa hedhi kwa wanawake hutofautiana ambapo baadhi mzunguko wao huchukua siku 24 wakati wengi huenda hadi siku 34.

Kufuatia kutofautiana huko, msichana anaweza kujiona kuwa ana tatizo, kumbe sio. Na utofauti huo katika mwezi unaweza kuwa ni kwa kipindi cha miaka michache tu tangu alipopata hedhi kwa mara ya kwanza.



Mwili wa msichana unaweza usifuate kikamilifu mzunguko wa hedhi hasa katika kipindi cha miaka miwili ya mwanzo, na jambo hili si tatizo. Wakati mwingine unaweza usipate hedhi au ukapata kwa kuchelewa tofauti na awali.

Ugonjwa, kupungua uzito ghafla au msongo wa mawazo vinaweza kusababisha mzunguko wa hedhi kuvurugika kwa sababu sehemu ya ubongo inayoshughulika na hedhi, huathiriwa na vitu hivyo.

Jambo jingine linalosababisha kubadilika kwa mzunguko kwa hedhi ni pamoja na kubadilisha ratiba yako au kusafiri kwenda katika mazingira mapya.

Mbali na mvurugano huo, idadi ya siku za msichana kutokwa na damu pia hutofautiana kutoka hedhi moja kwenda nyingine ambapo unaweza kupata hedhi kwa siku 3, lakini nyingine ikawa siku 7. Yote haya yanatokana na kiasi tofauti cha homoni ambacho mwili huzalisha kila mwezi.

Wasichana wengi ambapo mzunguko wao huvurugika huwa mara nyingi wanapata wakati mgumu kujua ni lini atapata hedhi ili aweze kujiandaa. Hapa chini ni baadhi ya dalili mwili wako                      utazionyesha kuwa unakaribia kupata hedhi;
                                                     Matiti kuongezeka uzito au kuuma
                                                     Maumivu ya kichwa
                                                     Kutokuwa kawaida (moods)
                                                     Maumivu ya tumbo
                                                     Kutokwa chunusi
                                                     Kuumwa/kukakamaa mgongo
                                                     Kutolala kawaida

Kuvurugika kwa mfumo wa hedhi ni jambo la kawaida hasa kwa wasichana katika miaka ya mwanzo ya hedhi, lakini kadiri umri unavyokwenda na mzunguko huo unazidi kuwa sawa sawa.

Lakini, baadhi ya wasichana wanaweza kuwa na kuvurugika kwa hedhi au wasipate kabisa kutokana na, kufanya mazoezi sana, kutumia dawa, kupungua kwa uzito sana au kutokula vyakula sahihi mfano, kalori ya kutosha, lakini pia kutokuwapo kwa uwiano sawa wa homoni ndani ya mwili.

Endapo mwili wa msichana utazalisha kwa wingi homoni ya androgen huenda ikasababisha tatizo hilo. Homoni hii huhitajika kwa wingi kwa mwanaume ili kusaidia kuota ndevu, nywele kifuani, sauti kuwa nzito, kujenga msuli.

Unashauriwa kumuona daktari endapo tatizo hili la kuvurugika kwa mfumo wa hedhi litaonekana kukusababishia matatizo zaidi au limekaa kwa zaidi ya miaka mitatu tangu ulipopata hedhi kwa mara ya kwanza.

Lakini pia unashauriwa kuonana na daktari kama ikitokea hujapata hedhi na huna ujauzito na pia endapo hedhi yako itakaa zaidi ya siku 7, au muone daktari kama umepata hedhi ndani ya kipindi cha muda mfupi tangu ulipopata mara ya mwisho.

Vinginevyo, unashauriwa kutembea na pedi kwa ajili ya kujikinga kama mzunguko wako sio ule ambao unatabirika kwamba utatokea lini.

Related Posts

Post a Comment